Habibu B. Anga Profile picture
Author| To Infinity and Beyond

Sep 4, 2021, 41 tweets

𝗞𝗔𝗕𝗟𝗔 𝗬𝗔 𝗜𝗞𝗨𝗟𝗨.. 𝗞𝗪𝗔𝗡𝗭𝗔 𝗔𝗗𝗛𝗔𝗕𝗨 𝗬𝗔 𝗞𝗜𝗙𝗢

Thread..

Ukiwa unatoka Lusaka kwenda Jimbo la Magharibi, kabla hujaingia mji wa Mongu kuna kipande cha barabara kinajulikana kama Limulunga Road.
Kipande hiki cha barabara mwaka juzi kimetupa tukio la kipekee

ambalo kwa kiwango kikubwa tukio hili limebadili mwelekeo wa siasa la bara zima la Afrika na hasa nchi za kusini mwa jangwa la Sahara.

Pengine pasipo tukio hili huyu Hichilema tunayemuona leo asingelikuwa Rais. Lilikuwa tukio la kipekee kabisa..

Kila mwaka pale Zambia huwa wana

sherehe maarufu zinaitwa "Kuomboka Ceremony".
Wenzetu mpaka leo hii bado wanatambua cheo cha asili cha "Litunga" ambaye ni Mfalme wa kabila la Walozi.
Kila mwaka mwishoni mwa msimu wa mvua mfalme huwa anahama kutoka makazi yake ya bondeni ya Lealui na kuhamia makazi yake yaliyo..

kwenye mwinuko, Limulunga
Utamaduni huu umekuwa unafanyika kwa muda wa zaidi ya karne tatu sasa
Maelfu ya wananchi waliovalia nguo za asili huwa wanakusanyika hapo Limulunga, kumpokea Mfalme Litunga akiwa anawasili. Kutokana na umashuhuri wa tukio hilu, hivyo huvutia watu maarufu

wanasiasa mpaka viongozi wakuu wa nchi.

Sasa, kwenye sherehe za Kuomboka za mwaka 2017 tukio la ajabu sana lilitokea.

Hakainde Hichilema na wafuasi wake wakiwa na msafara wa magari kama kumi hivi walikuwa wanasafiri kutoka Lusaka kwenda kwenye hizi sherehe.
Lakini walipofika...

barabara ya Limulunga kilomita chache tu kabla ya kuwasili eneo la tukio, wakasikia ving'ora vinalia nyuma yao na gari za polisi zikiwa zunakuja kwa kasi ya ajabu

Ving'ora hivi vya polisi vilikuwa vinaendeshwa katika mtindo wa kuashiria kwamba msafara wa kiongozi wa nchi ulikuwa

unapita na hivyo Hichilema na msafara wake wanatakiwa wakae pembeni ya barabara ili msafara wa Rais Edger Lungu upite.

Huyu Huchilema usimuone na sura yake hii ya upole. Ni mtu mwenye msimamo mkali hasa na thabiti.

Akawaelekeza madereva wa msafara wake kwamba wasiupishe msafara

wa Lungu badala yake waendelee kuendesha magari katikati ya barabara.
Akasema kwamba hawakupewa taarifa yoyote juu ya msafara wa Lungu na kwa mujibu wa protokali, Lungu anatakiwa kuingia eneo la tukio mtu wa mwisho. Hivyo msafara wake unatakiwa kuwa nyuma yao.

Tunakumbuka namna

ambavyo Rais Lungu alikuwa na ulinzi mkali uliopitiliza. Kwenye msafara wake alikuwa mpaka na gari za NSTV (zile gari kama pickup alafu juu ina machine gun au rotary cannon)
Kwa hiyo baada ya kuona msafara wa Hichilema hauwapishi, ving'ora vya polisi pamoja na hizi NSTV wakatoka

nje ya barabara na kisha wanaendesha kuingia ndani ya barabara kama wanakuja kuwagonga akina Hichilema kuwatoa barabarani.
Lakini Hichilema akawasisitiza madereva wake wasiogope.. wakanyage mafuta hakuna kumpisha mtu.

Baada ya kuona kwamba hakuna wanachoweza kufanya kumtisha..

Hichilema na msafara wake, ikabidi magari ya msafara wa Rais Lungu utembee pembezoni mwa barabara (tairi moja nje ya barabara, tairi moja ndani ya barabara) na kuupita msafara wa Hichilema ambao bado ulikuwa unatembea katikati ya barabara.

Kwa hiyo msafara wa Rais Lungu ukawa wa

kwanza kufika eneo la tukio

Eneo lenyewe la tukio ni sehemu ya wazi. Yaani chukulia mfano kama pale Jangwani pembezoni mwa mto Msimbazi. Unafunga barabara Magomeni Mapipa na Fire kwa kuweka uzio wa muda.Alafu maelfu ya watu wanajaa pale jangwani kumsubiri Mfalme ambaye atawasili

na mashua kwa kupitia mto msimbazi.

Kwa hiyo baada ya Rais Lungu kuwasili na kuketi eneo aliloandaliwa, walinzi wake wakiwa na mitutu wakachukua jukumu la kuweka ulinzi eneo la kuingilia hapo kwenye sherehe.

Dakika chache baadae, Hichilema akiwa na msafara wake nao wakawasili..

Pale kwenye eneo la kuingilia wakakuta walinzi wa Rais Lungu wenye mitutu ya bunduki wakiwaeleza kwamba hawawezi kuingia ndani.
Hichilema alipouliza kwa nini hawawezi kuingia, walinzi wa Rais wakajibu tu kwamba wana maagizo kwamba wasimruhusu mtu mwingine yeyote kuingia baada ya

Rais kuwa ameshawasili

Hichilema akaanza kubishana nao akiwaeleza kwamba hilo sio tukio la kiserikali bali ni tukio la kimila liko chini ya Walozi, Rais Lungu amehudhuria kama mwananchi mwingine yeyote yule kwa hiyo hawana mamlaka yoyote ya wao watu wa serikali kuweka masharti..

ya kutaka kuruhusu nani aingie au nani asiingie. Mamlaka hayo wanayo walozi na mfalme wao pekee.

Licha ya hoja hizo, walinzi wa Lungu wakaendelea kushikilia msimamo kwamba wamepewa amri wasiruhusu Hichilema aingie.

Ili kuepusha kuharibu shughuli hii, Hichilema akarejea kwenye..

gari yake. Japo hakuondoka. Akaa ndani ya gari kutafakari wafanyaje na kutuliza munkari wa wananchi ambao walikuwa wameshajaa kutaka kuwashambulia walinzi wa Lungu.

Kama nusu saa baadae kwa ajabu kabisa, ghafla kelele na vifijo vilisikika kutoka uwanjani kwenye eneo la tukio..

walinzi wa Hichilema haijulikani walitumia ujasusi gari, lakini walifanikiwa kumpenyeza kwa siri Hichilema akaingia ndani bila walinzi wa Lungu pale getini kujua.

Hichilema alipoingia ndani uwanja mzima ulilipuka kwa shangwe wahudhuriaji wakimshangilia "RAIS.. RAIS... RAIS..!!"

Shangwe zilikuwa kubwa kiasi kwamba mpaka Hichilema ilibidi awatulize wahudhuriaji kuwataka wawe watulivu kwa heshima ya kumsubiria Mfalme Litunga

Muda kidogo baadae Mfalme Litunga akawasili na mashua zake nne kama ilivyo tamaduni. Mbele imetangulia mashua ya walinzi wake, kisha

mashua yake inayojulikana na walozi kama 'nalikwanda' yenye sanamu ya tembo juu na moshi ukiwa unafuka toka ndani kuashiria kitamaduni kwamba Mfalme yu hai na buheri wa afya.
Nyuma yake inafuata mashua ya malkia yenye sanamu ya ndege yange yange kwa juu na nyuma boti ya walinzi..

Mfalme akawasalimu wageni mashuhuri akina Hichilema na kisha Lungu, na kisha kuketi kabla ya kuanza kuwahutubia watu wake.

Mfalme Litunga alipomaliza kuhutubia, Edger Lungu akafanya kitu cha ajabu kabisa. Akaomba nafasi naye ya kuzungumza.

Lakini alipoanza tu kuzungumza...

Hichilema na wapambe wake wakainuka na kuanza kuondoka.
Alipoinuka tu, umati wa watu ukalipuka tena kwa shangwe na kuanza kumshagilia, "..RAIS... RAIS... RAIS... RAIS.!!"

Na sio tu kwamba walikuwa wanamshangilia, bali walikuwa wanamfuata akiwa anaondoka.
Wananchi walikuwa...

wanaondoka pamoja na Hichilema wakiwa wanatoa maneno makali kumkejeli Lungu kwamba wamekuja kwa ajili ya Mfalme na si yeye, sasa anahutubia kama nani?
Ili kuokoa jahazi ilibidi Lungu aombwe akatishe hotuba yake ili wananchi wasiondoke, lakini walichelewa, msafara wa Hichilema..

ulikuwa umeshaanza kuondoka na wananchi walikuwa wanamkimbilia huku wakiendelea kumshangilia.

Sikukuu ya "Kuomboka" ya mwaka 2017 iliisha kwa drama namna hii. Rais Lungu akipata aibu na Hichilema akiwa shujaa.

Kitendo hiki kilimuuma mno mno Rais Lungu
Kwanza Hichilema kukataa..

kupisha msafara wake. Na pili namna ambavyo wananchi walimzomea yeye na kumshangilia Hichilema wakimuita "RAIS".!
Lungu aliumia haswa na akajiapiza kumshugulikia.

Siku mbili tu zilipopita, vikosi vya jeshi la polisi pamoja na maafisa wa idara ya Ujasusi wakiwa na silaha nzito..

Walifika nyumbani kwa Hichilema.
Mwenyewe hawakumkuta kwa hiyo wakawaweka chini ya ulinzi wafanyakazi wake wote. Kuanzia walinzi wake mpaka wasaidizi wa kazi za nyumbani.

Wakawakusanya sebuleni na kuanza kuwahoji huku wakiwashushia kipigo waseme Hichilema yuko wapi
Wote wakajibu

Hawajui.

Maafisa wa polisi walienda mbali zaidi na kuanza kuwabana kwa 'plaizi' sehemu za siri vijana hawa.

Moja ya wasaidizi wa Hichilema akashindwa kustahimili maumivu na kuwaambia maaskari kwamba kuna chumba cha siri ndani ya nyumba hiyo. Akawapeleka na kuwaonyesha...

Chumba hiki kilikuwa na malango mzito ambao ulikuwa ukifungwa kwa ndani huwezi kuufungua nje.
Kwa dakika kadhaa polisi wajaribu kuuvunja bila mafanikio.

Baada ya muda wakafanikiwa kutengeneza tobo kwenye mlango.
Wakatumia tobo hili kupiga mabomu ya machozi kwenda ndani ya hiki..

Chumba.

Ndani ya hiki chumba walikuwa wamejificha Hichilema, mkewe na mtoto wao mdogo wa mwisho.

Mabomu yalipigwa mengi kiasi kwamba ndani kukawa na wingu zito mpaka wakashindwa kupumua.
Mkewa Bi. Mutinta ambaye ni mgonjwa wa asthma wa muda mrefu akadondoka na kupoteza fahamu..

Sekunde kadhaa baadae, mtoto wake naye akadondoka na kupoteza fahamu.
Ili kuokoa uhai wa mkewe na mtoto Hichilema ilibidi afungue mlango

Alipofungua tu mlango akadakwa na maafisa wa polisi na kubebwa mzobe mzobe mpaka kwenye karandinga na kisha wakatokomea naye

Kwa muda wa siku

nane, Hichilema alishikiliwa gereza kuu la Lusaka kwenye solitary confinement akiteswa na kulazimishwa kukiri mashitaka kadhaa
Hichilema mwenyewe anasema walikuwa wakimpiga na kumpulizia pilipili kali kwenye uume

Ndani ya siku hizi nane mkewe alifika mara kadhaa gerezani kumuona

Lakini alifukuzwa.

Marehemu Mzee Kaunda naye alijitosa kwenye sekeseke hili kwa kwenda hapo gerezani kumuona Hichilema, lakini naye alifukuzwa kama kibaka.
Kiongozi wa chama cha DA cha Afrika Kusini alipoingia Zambia kujaribu naye kwenda kumuona Hichilema, yeye alifukuzwa uwanja

wa ndege kabisa hakuruhusiwa hata kushuka kwenye ndege.

Hali ilikuwa tete kiasi kwamba Afrika Kusini ikaanza kutishia kusitisha uhusiano wao na Zambia.

Baada ya presha kuwa kubwa ndipo mwendesha mashtaka wa serikali akamfungulia mashtaka rasmi Hichilema.
Ajabu mashataka ambayo

walimfungulia, yalikuwa ni ya uhaini

Walidai kwamba, kitendo cha Hichilema kukataa kupisha msafara wa Rais, alikuwa kwa makusudi kabisa anahatarisha usalama wa Rais. Kwa hiyo lilikuwa ni jaribio la kudhuru uhai wa Rais, na hivyo ni kosa la uhaini

Pale Zambia mashataka ya uhaini

yanabeba adhabu ya juu ya kifungo cha maisha au kunyongwa.

Kwa hiyo, kiongozi wa Upinzani alikuwa kwenye hatihati ya kuhukumiwa kunyongwa.

Mashataka haya yaliposomwa, ulimwengu ulizizima.

Jumuiya za kimaifa, Marekani, Umoja wa Ulaya, Jumuiya ya madola wote walimkalia kooni..

Rais Lungu kumtaka serikali yake ifute mashtaka dhidi ya Hichilema.

Mbaya zaidi baada ya mashtaka haya kusomwa tu, Rais Lungu alikuwa ametangaza hali ya hatari nchi nzima ili kuwadhibiti wananchi ambao walikuwa wanataka kuandamana

Mvutano kati ya serikali ya Lungu na Jumuiya ya

Kimataifa ulidumu kwa miezi minne huku Hichilema akiendelea kusoma gerezani.

Baada ya presha kuwa kubwa kwa Rais Lungu, hatimaye baada ya miezi minne Hichilema akaachiwa huru.

Kama una ndugu au jamaa anaishi pale Zambia hebu muulize hii siku ilikuwaje.
Nchi nzima ilizizima kwa

shangwe. Jiji la lusaka lilifurika maelfu kwa maelfu ya watu waliojitokeza barabarani kuulaki msafara wa Hichilema akiwa anatoka gerezani.

Hichilema aligeuka kuwa shujaa mpya wa Wazambia.

Umaarufu wake ndani ya nchi na kimataifa ukapaa viwango vya juu kabisa angani.

Hichilema akawa tumaini jipya

And the rest is history.. tunajua nini kilitokea.Juzi hapa hatimaye rasmi sasa Wazambia wamemkabidhi nchi Hichilema awe kiongozi wao mkuu

Ukitafakari, utajiuliza kwa nini hizi nchi zetu kusini mwa jangwa la Sahara kwa muda wa miaka 60 karibia zote

zipate uhuru ni kama hatujapiga hatua yoyote.

Moja ya shida yetu kubwa ni kwamba hatujifunzi toka kwenye historia.
Kile kilichotokea Zambia utakiona ni hicho hicho kinatokea kwenye nchi nyingine hapa Afrika Mashariki.

Watesi na wanaoteswa wana cha kujifunza toka Zambia na huu..

Hakuna anayeijua kesho, tumia cheo vyema kuinua jamii.

Haijalishi usiku ni mrefu kiasi gani, au unatisha kiasi gani, au una majinamizi gani. Ifikapo asubuhi, lazima.. lazima jua lichomoze. Lazima nuru itaonekana. Hii ni kanuni ya kwanza ya maisha.

Habib
To Infinity and Beyond

Share this Scrolly Tale with your friends.

A Scrolly Tale is a new way to read Twitter threads with a more visually immersive experience.
Discover more beautiful Scrolly Tales like this.

Keep scrolling